MCHAKATO WA KUIGEUZA BODI YA UTALII KUWA MAMLAKA YA UTALII UHARAKISHWE– BALOZI MULAMULA


Balozi wa Tanzania nchini Marekani Mh. Liberata Mulamula ametoa rai kwa vyombo vinavyohusika kuharakisha mchakato wa kuigeuza Bodi ya Utalii (TTB) Tanzania kuwa Mamlaka ya Utalii Tanzania ili kukiwezesha chombo hili kuwa na uhuru zaidi na uwezo mkubwa katika kutangaza vivutio vya utalii na kusimamia sekta ya utalii nchini.
Hayo yalisemwa na Balozi Mulamula hivi karibuni alipomtembelea Mkurugenzi Mwendeshaji wa Bodi ya Utalii Tanzania Dk. Aloyce K. Nzuki ofisini kwake  ili pamoja na mambo mengine kuzungumza namna gani Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani utasaidia juhudi za TTB katika kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania katika soko la Marekani.“Ni muhimu ifike mahali TTB iwe na nguvu kisheria na uwezo zaidi katika  kutekeleza majukumu yake  bila kuingiliwa au kuwepo kwa migongano, hivyo ni vema mchakato huo wa mageuzi ukaharakishwa” alisema Balozi Mulamula.
 Akifafanua zaidi kuhusu suala hilo Dr. Aloyce Nzuki alisema tayari Bodi ya Utalii ilikwishaandaa andiko kuhusu kuigeuza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kuwa Mamlaka ya Utalii Tanzania (TTA) na andiko hilo kwa sasa liko Wizarani.
Aidha balozi Mulamula ameipongeza TTB kwa kubuni onesho la utalii liitwalo Swahili International Tourism Expo (S!TE) litakalo kuwa likifanyika kila mwaka mwezi Oktoba ambalo litatumika pia kuonesha utamaduni wa mwambao na kukuza lugha ya Kiswahili. Ameahidi kuweka kiunganisho (link) cha tovuti ya onesho hilo la S!TE katika tovuti ya Ubalozi. Sambamba na hilo amesema pia kuwa kuanzia mwaka huu ofisi yake ambayo imekuwa ikiandaa na kuratibu safari ya wafanyabiashara mashuhuri wa Marekani kutembelea Tanzania (VIP Safari) sasa itakuwa ikiandaa safari hiyo na kuwaleta wafanyabiashara hao mwezi Oktoba wakati wa onesho hilo la S!TE badala ya utaratibu wa zamani wa kuwaleta wakati wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es salaam maarufu kama Sabasaba.
Ameahidi kuwa ubalozi wa Tanzania nchini Marekani utafanya kila liwezekanalo kusaidia juhudi za TTB katika kuitangaza Tanzania kama eneo zuri la utalii duniani na akaiomba TTB kuendelea kuwapa taarifa mbalimbali za vivutio vya utalii kadri iwezekanavyo ili kuwasaidia kutekeleza azma hiyo.

No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.