USAJILI MAOMBI YA VITAMBULISHO VYA TAIFA WAANZA MKOA WA MOROGORO
Mamlaka
ya Vitambulisho vya Taifa(NIDA) Imeanza rasmi zoezi la Usajili na
Utambuzi wa Watu Mkoa wa Morogoro pamoja na uchukuaji alama za vidole,
picha na saini ya kielektroniki kwa wananchi wa Wilaya ya Kilombero
ambao zoezi la Ujazaji fomu za maombi ya vitambulisho lilishafanyika.
Kuanza kwa usajili na Utambuzi wa
Watu mkoa wa Morogoro kumefuatia kukamilika kwa zoezi kama hili mikoa ya
Pwani, Lindi na Mtwara ambapo sambamba na usajili unaoendelea sasa
mkoani Morogoro zoezi la uchukuaji alama za vidole picha na saini ya
kielektroniki limekuwa likiendelea katika baadhi ya Wilaya za mkoa wa
Pwani.
Mkoani Morogoro; katika eneo la
Mikese kijiji cha Fulwe tumeshuhudia msururu wa watu wakisubiri
kusajiliwa huku wengine wakiwa katika harakati za kuingizwa katika
Rejesta ya Makazi inayomilikiwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa na
Vijiji. Kwa utaratibu wa sasa ili uweze kusajiliwa lazima kwanza kuwa
unatambulika katika serikali yako ya Mtaa/Kijiji na kuwa umeorodheshwa
katika Rejesta ya Makazi ya Mtaa au Kijiji husika.
Leo ikiwa ni siku ya kwanza ya
kuanza kwa zoezi hilo litakalodumu kwa siku saba mpaka Jumapili ya
tarehe 29/09/2014 wananchi wengi wameonekana kuhamasika na kujitokeza
kwa wingi katika siku ya kwanza tofauti na mazoea ya wengi kujitokeza
siku za mwisho za zoezi.
Changamoto kubwa bado imebaki
wananchi wengi kukosa Viambata msingi vya kuwatambulisha kama vyeti vya
kuzaliwa, vyeti vya elimu ya msingi au sekondari n.k jambo ambalo
limekuwa likisisitiziwa sana na NIDA katika kurahisisha utambulisho wa
mwombaji. (Picha na Rose Mdami- NIDA)
Leave a Comment