Unajua ni kwanini wanaume hupenda kuangalia wanawake wengine hata wawapo na wapenzi wao?

 
Inatokea unapata mtoko na mpenzi mpya na baada ya kubadilishana anuani za mawasiliano zikiwemo zile za mtandaoni unapata tashwishwi ya kuingia katika ukurasa wake wa facebook. Lahaula, huko unakutana na picha kedekede za wanawake warembo hasa na wenye sifa za kugombea mashindano ya ulimbwende.
Unashikwa na udadisi na siku mnapokutana swali lako la kwaza ni kutaka kujua wale ni akina nani. Na yeye bila ya wasiwasi anakujibu kwamba ni marafiki zake tu wa mtandaoni na wala hajawahi kukutana nao zaidi ya kuwasiliana kwa njia hiyo ya mtandaoni.
Lakini kama mjuavyo wanawake walivyo, majibu hayo hayaoneshi kumridhisha, hivyo anaendelea kudadisi zaidi ili kujiridhisha, na si ajabu maswali yakawa mengi kulingana na namna majibu yatakavyokuwa……………..
Ukweli ni kwamba ni vigumu kwa mwanamke kupokea majibu mepesi hasa pale linapotokea jambo analolitilia mashaka, ni lazima atahisi kuna kitu kinaendelea…………..
Wakati mwingine inaweza kutokea mwanamke yuko na mpenzi wake wamekaa mahali au wako kwenye mtoko, mara akapita mwanamke, na ghafla akamuona mpenzi wake anageuza shingo na kumkodolea macho, wakati mwingine mwanamke anaweza kupuuza, lakini inaweza kutokea kila anapokatiza mwanamke katika eneo hilo, mwanaume anageuza shingo na kumkodolea macho……………..
Kitendo hicho kinaweza kuibua maswali kutoka kwa mwanamke. Na kama mwanaume asipotoa majibu ya kuridhisha kwamba ni kwa nini macho yake yako juu juu kutazama wanawake, kuna uwezekano wa kuzuka tafrani.
Hebu ngoja niwamegee siri, sababu inayotufanya tuwe tunawaangalia wanawake hususan wanawake warembo ni kwa sababu wanaume wanapenda kuangalia wanawake warembo. Wanaume huwa tunapenda kuangalia picha za wanawake warembo, senema zinazoonyesha wanawake warembo, mashindano ya ulimbwende yanayoshirikisha wanawake warembo, yaani tumezaliwa na kukuzwa kwa umri na kimo katika mazingira hayo….
Wanawake, kamwe msidhani kwamba kuwakodolea macho wanawake warembo na labda kutokwa na udenda ndio tunataka kulala nao….. La hasha, tunasafisha kiwi cha macho tu na maisha yanaendelea…………..
Ni vyema jambo hilo mkalichukulia kama kitu cha kawaida. Kama utakuwa na mpenzi ambaye haangalii wanawake warembo wapitao mbele yake. Bila shaka utakuwa una mpenzi au mume mwenye kasoro…. huyo hatakuwa ni mtu wa kawaida………!
Hatuna mawasiliano nao, wala hatufanyi kitu chochote na wao, zaidi ya kuwaangalia tu na kuwaacha kama walivyo, sasa ya nini mpate jakamoyo na kujipa presha.
Wanaume tunapenda kuangalia wanawake, yaani hilo halina mjadala, inabidi tu mkubaliane na hali halisi kwa hiyo siku nyingine ukimuona mpenzi wako au mumeo anaangalia wanawake warembo wala usijisumbue kugombana naye kwa maswali kwani hali hiyo itamfanya wakati mwingine awe anakandamiza hisia hizo za kuangalia wanawake wengine na kama mjuavyo mtu akikandamiza jambo kwa muda mrefu mwishowe hulipuka na ushawishi wa kwenda mbali zaidi unakuwa ni mkubwa. (kukandamiza maana yake ni kujizuia kwa nguvu zote kufanya jambo au kitu ambacho unatamani sana kukifanya kwa kuhofia kama watu waliokuzunguka watakuonaje, kwa mfano kufanya ngono, kunywa pombe, kuvuta sigara, nk).
Hivyo basi msije tutoboa na vidole vya macho, kwani mwanaume anapowaangalia wanawake warembo huwa anaishia kuangalia kwa macho tu, lakini moyo wake uko kwako……………LOL

No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.