STORI ITAKAYOKUFANYA UJIONE UMECHELEWA



 
Umakini unahitajika sana hasa pale mwanaume unapotafuta mwanamke wa kuanzisha nae maisha, simulizi hii nimeiona mahala nikaona bora nijaribu ku share nanyi.
Desemba 22, 2007. Jumamosi.
Victor, akiwa na miaka 36, alikuwa akifunga ndoa. Ilikuwa ni siku ya sherehe hoi hoi nderemo na vifijo kwani wengi wetu tulikuwa tumeshahisi kuwa kaka Victor hatooa tena. Kila siku alikuwa akituambia kuwa anajipanga na maisha, na anawaandalia watoto wake maisha mazuri.
Tulibaki tukijiuliza hao watoto wako wapi maana hatuoni hata dalili za yeye kuwa na ukaribu na mabinti hata wa jirani.
Kaka Victor kwa jina lingine Mchungaji ni katika wale wakaka ambao wakati tunakua walikuwa ndio wakaka wa kutolewa mifano majumbani mwenu (role models). Yaani ukifanya jambo baya au kosa unaambiwa, “Muangalieni kaka yenu, kwa nini msimuige hata robo tu ya tabia zake?”
Kuna kipindi rafiki yake aliwahi kuniambia, “Yani siku nikimkuta mchungaji Victor na mwanamke chumbani na wote wako uchi na mchungaji akaniambia, sijamfanya chochote, nitamuamini”
Hivyo ndivyo jinsi kaka Victor alikuwa amejijengea sifa katika jamii. Zaidi ya yote, kaka Victor alikuwa mfano wa kuigwa hata kimasomo kwani baada ya kumaliza shahada yake ya kwanza katika masomo ya uchumi na kufaulu vyema, alibahatika kupata ufadhili wa kwenda kusoma masomo ya shahada ya uzamili katika chuo kikuu cha Havard huko Massachussets, nchini Marekani.
Alikuwa na akili ya peke yake na mtu wa kujituma. Kwani alipomaliza chuo yeye kabla hata chuo kikuu cha Dar es salaam hawajamuita kuwa mkufunzi msaidizi alikuwa ameshajiajiri kwenye kampuni yake ndogo ya BIMA.
Ngoja nikurudishe nyuma kidogo; wakati yuko mwaka wa pili chuoni yeye pamoja na mwenzake waliandika proposal ambayo ilishinda na walipewa kila mtu fedha taslimu shilingi milioni tano. Katika vitu alivyovifanya ilikuwa kununua kiwanja huko Kigamboni jijini Dar es salaam, eneo kubwa huko ambako kwa sasa kuna kijiji kiitwacho Avic town.
Fedha nyingine alianzisha ‘agency’ yake ya mambo ya BIMA. Ni wakati anajiandaa kwenda kusoma nje alipofuatwa na wawekezaji waliojenga hiyo Avic town ili wanunue eneo lake kwani lilikuwa limepakana sana na eneo lao.
Kwa fedha zile aliwekeza zaidi kwenye ‘agency’ yake na kuongeza mtaji hadi kufanikiwa kuwa ‘brokerage’. Pamoja na yote hayo alikuwa na vibiashara vya hapa na pale ambavyo vilifanya maisha yake mjini hapa kuwa mazuri na alizidi kutufanya wadogo zake sisi tuonekane bado sana.
Kaka Victor alikuwa mcheshi na mchangamfu na kama kawaida wadada wengi walijisogeza kwake lakini nahisi katika mambo yaliyokuwa mwishoni mwa mawazo yake ni hilo la wanawake.
Kila alipokuwa akiulizwa suala la mahusiano alijibu, tena kwa kizungu, “I worry about things that I have to struggle for, not those that are provided by nature” akimaanisha yeye anahofia juu ya mambo ambayo inabidi kuyapigania kuyapata na sio yale ambayo yapo tu.
Kwamba siku mtu akitaka kuoa ataoa tu lakini huwezi kutaka kuwa na mali na ukawa nazo, lazima uweke bidii kuzipata. Akiulizwa na watu wazima zaidi kuhusu ndoa alikuwa akijibu, “najipanga na kuwaandalia maisha wanangu."
Siku zote hakukosa jibu la kwa nini hakutaka kuoa na kwa hilo alifanikiwa kwani alifanikiwa kuwa na biashara ambazo zilikuwa zinaenda vizuri, nyumba ya kuishi na nyingine za kupangisha tena si kwa hela zetu za madafu, uwezo wa kubadili magari japo si kwa kila siku n.k.
Siku kaka Victor anatuambia anataka kuoa hakuna aliyeamini, hata alipomleta binti ambaye kwa hali ya kawaida wengi tungemkataa basi ilibidi tutafute justifications (vihalalishi) za kuonesha kuwa anaweza kuwa wa tofauti.
Na siku ya Jumamosi, Desemba 22, 2007 kaka Victor alifunga pingu za maisha huku akiwa kwa hakika amejiandaa na kujipanga vyema kwa ajili ya wanae ambao sasa tuliona wanaweza kupatikana.
Kuanzia Januari 2009
Mafanikio yalizidi kumiminika kwa kaka Victor ambapo wakati huu Mungu alikuwa amewabariki na mtoto mmoja, James. Ni wakati huu pia alipopata ufadhili kwenda nchini Ufaransa kwa ajili ya shahada yake ya uzamivu.
Aliondoka akiwa na amani kabisa akijua kuwa kila kitu amekiacha kikiwa katika mikono salama. Hadi wakati kaka anasafiri hatukuwa na ukaribu sana na shemeji yetu – mke wake – kwani hakupenda sana kututembelea na wala hakuwa akipenda tukienda kwake.
Hata hivyo tulimheshimu kwani kaka alikuwa akimpenda sana na kumuamini. Mwezi wa tano kaka alinipigia simu kuwa amepata safari kwenda jijini Rio de Janeiro kwa ajili ya mkutano. Nilimtakia kila la kheri na hata alipofika alinieleza jiji hilo lilivyo zuri na kunitumia baadhi ya picha kupitia barua pepe.
Juni, 1 2009
Nilipata habari kuwa ndege ya Air France iliyokuwa ikitokea Rio de Janeiro kuelekea jijini Paris imepata ajali na abiria wote 216 waliokuwamo wamefariki. Kwanza haikuniingia akilini hadi nilipokumbuka kuwa hiyo ndiyo siku ambayo kaka alikuwa asafiri kurudi chuoni kwake huko Ufaransa.
Nilijikuta nikisali kumuomba Mungu kaka asiwepo kwenye ndege hiyo. Nilijaribu kutumia njia mbalimbali kuhakiki kama alikuwepo bila mafanikio yoyote. Ni hadi walipotangaza orodha ya abiria waliokuwa wamepanda ndege ile ndipo tulipofahamu kuwa kaka Victor hatunaye tena duniani.
Mipango ya mazishi ilifanyika na kwa kuwa miili yao haikupatikana – kwani ndege iliangukia baharini – tulifanya tu ibada na kila mtu kutawanyika.
Tulimuuliza shemeji kama aliacha wosia wowote na kama ilivyo ada hakuwa ameandika chochote isipokuwa tu kwa kutumia fomu alizokuwa akijaza kazini na kwingineko alikuwa akimuandika mkewe kama mrithi pekee wa mali zake endapo kifo kitamkuta.
Hivyo sisi kwa kuamini walikuwa wanapendana hatukuona shida na tulimsaidia kupata vibali vyote vya kuhakikisha mirathi na stahiki zote za mumewe anazipata yeye. Tulimuonea sana huruma shemeji yetu kwani bado alikuwa binti mdogo.
Januari 6, 2016
Mpaka naandika hapa, shemeji yetu, aliyekuwa mke wa kaka yangu Victor, amehamia nchini Uganda ambako ameolewa na mwanaume aliyekuwa akifanya kazi ubalozi wa Tanzania nchini Uganda.
Miezi kama miwili tu baada ya kaka kufariki, shemeji alitokomea kusikojulikana na kumuacha James mwanaye kwa mama yetu. Tulipojaribu kufuatilia mali za mumewe alizoziacha tulikuta zote zimeshabadilishwa umiliki na hata kampuni ndogo ile ya BIMA aliiuza kwa mchaga mmoja bila taarifa kwetu.
Hakurudi kumuangalia mtoto na hata alipokutana na ndugu yetu mwingine alisema yeye ni mdogo mno kukaa peke yake na huyo mtoto anamnyima fursa hivyo hatomrudia.
Ni jana tu ndiyo nilitoka kumlipia ada James ili aweze kuanza darasa la kwanza mwaka huu. Hua najiuliza ni aina gani ya Mke kaka Victor alipata, yote aliyokuwa akituambia kuwa anatafuta pesa kwa ajili ya mwanae ndio yameishia hivi kwa sisi kumtunzia Mwanae. Juhudi na maarifa yake yote imekuwa bure kabisa. Mwanae hatafaidi jasho lake hata kidogo.
KUMBUKA
MAISHA YANA MITIHANI MIKUBWA SANA JIFUNZE KUPITIA MITIHANI WANAYOPITIA WENZAKO ILI SIKU UKIKABILIANA NA MTIHANI WOWOTE ULE UJUE NI JINSI GANI YA KUWA MVUMILIVU NA KUWEZA KURIKABILI

No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.