TAARIFA YA HABARI YA LEO JANUARY 18 PLANET FM HII HAPA



18.01.2014           SAA 1:00 USIKU       UTAFITI
MWANZA
Utafiti uliofanywa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa), umebaini kuwa jamii bado inaficha kesi za ukatili kutokana na mila na desturi za Waafrika zilizojengeka miongoni mwao.
Utafiti huo umebainishwa na Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Bukoli iliyoko mkoani hapo, Christian Mwalimu, ambapo amesema kesi nyingi za kutelekeza familia, vipigo na unyanyasaji kwa wanawake, hukosa ushahidi kutokana na mlalamikaji kupewa vitisho vya maisha yake.
Amesema kuwa wanapokea kesi nyingi za ukatili wa kijinsia, hasa za manyanyaso ndani ya ndoa kwa mwanamke, kesi ambazo mara nyingi hazitolewi hukumu kutokana na mlalamikaji kushindwa kutoa ushirikiano na mahakama.
Aidha amesema, mila ni tatizo kubwa, kwakuwa wanawake waliumbwa kuwa wavumilivu hivyo kutokana na mila hizo wanalazimishwa kuishi kwa uvumilivu katika ndoa zao.

                        MWISHO




18.01.2014         SAA 1:00 USIKU       UKAGUZI
DODOMA

Waziri mkuu wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mh.Mizengo Pinda amesema ameridhishwa na kazi ya ukarabati inayoendelea kwenye maeneo mbalimbali ya jengo la Bunge ikiwa ni maandalizi kwa ajili ya Bunge lijalo la Katiba mpya.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo asubuhi wakati akipokea maelezo ya ukarabati kutoka kwa Mhandisi Mkuu wa Ofisi ya Bunge, Eng. Dk. Philemon Mzee, ambaye alikuwa akimtembeza kwenye maeneo mbalimbali yanayofanyiwa ukarabati ndani ya jengo hilo.

Dk. Mzee amemweleza Waziri Mkuu kwamba wanatarajia kuweka viti 670 vya wajumbe wa kawaida pamoja na viti 24 kwa ajili ya wajumbe wenye mahitaji maalum kama ya walemavu na mengineyo.

Katika ukumbi huo viti vya Spika na Makatibu wa Bunge pamoja na mfumo wa vipaza sauti umekamilika na kwamba kila kipaza sauti kimoja kitakuwa kinatumiwa na watu wawili kulingana na mpangilio wa ukaaji ulivyo hivi sasa.

Kwa mujibu wa Dk. Mzee, ukarabati huo unatarajiwa kukamilika Januari 30, mwaka huu ili kuweza kufanikisha zoezi zima la bunge la katiba kwenda kama ilivyo kusudiwa.


                MWISHO




18.01.2014        SAA 1:00 USIKU     USHIRIKIANO
DAR-ES-ASALAAM
Serikali ya Tanzania imedhamiria kuimarisha ushirikiano baina yake na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika Nyanja mbali mbali za miundombinu.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mh. Samuel Sitta wakati akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam.
Mh.Sitta amebainisha kuwa mwishoni mwa mwaka 2013, Mawaziri wa Tanzania, Burundi, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo walikutana kujadili namna ya kuimarisha miundo mbinu ya barabara, reli,anga na maji.
Aliongeza kuwa katika kikao hicho ilikubaliwa kuwa, Shirikika la ndege la Tanzania (ATCL) lipanue huduma zake na kufika nchini Burundi ambapo lilianza kufanya safari zake kati ya Tanzania na Burundi Desemba16, mwaka jana mara tatu kwa wiki, kama hatua za awali za utekelezaji.
Aidha katika mkutano wa 8 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya hiyo, umeridhia mfumo wa himaya moja ya Forodha na mpangokazi unaoainisha masuala ya utekelezaji katika kipindi cha miezi sita, ili kuwezesha kuanzishwa kwa himaya ifikapo Juni 2014.

                          MWISHO

 

 

18.01.2014      SAA 1:00 USIKU     VIFO

CAIRO
Waziri wa afya nchini Misri amesema kuwa, idadi ya watu waliofariki katika ghasia za kisiasa wakati kura ya maamuzi kuhusu katiba mpya ilipokuwa inaendelea imefikia watu 4 huku wengine 15 kujeruhiwa siku ya jana.
Ghasia hizo zilianza baada ya wafuasi wa aliyekuwa Rais wa Misri Mohammed Morsi kuandamana mjini Cairo, na katika mikoa mingine wakiilaani rasimu ya katiba inayopigiwa kura nchini humo.
Polisi nchini humo walilazimika kufyatua gesi ya kutoa machozi hewani ili kuwatawanya waandamanaji hao, ambao hawakuwa na kibali cha kuwaruhusu kufanya maandamano.
Tangu mapinduzi ya kijeshi yaliyomwondoa mamlakani Mohammed Morsi mwezi Julai mwaka jana, wanaharakati wa vuguvugu la Muslim Brotherhood, wamekuwa wakifanya vurugu kuipinga serikali ya mpito wakisema kuwa sio ya halali.
                                            MWISHO





18.01.2014     SAA 1:00 USIKU      SHAMBULIZI

KABUL
Watu 16 wameuawa wakiwemo wafanyakazi wanne wa Umoja wa Mataifa, katika mlipuko wa bomu na shambulizi la risasi lililofanywa kwenye hoteli moja nchini Afghanistan.
Taarifa zinasema kuwa mlipuaji wa kujitoa mhanga amejilipua nje ya mgahawa uliokuwa umejaa raia wa kigeni na wa Afghanstan, wakati watu wengine wawili waliokuwa na bunduki waliingia ndani na kuanza kufyatua risasi kiholela.
Mkuu wa polisi mjini Kabul, Jenerali Mohammad Zahir amesema watu 16 waliouawa wote walikuwa ndani ya mgahawa huo ambapo raia wa kigeni na wa Afghan ni miongoni mwa waliouawa.
Aidha katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon amethibitisha na kusema kuwa, mwakilishi wa Shirika la Fedha Ulimwenguni – IMF nchini Afghanistan  Bw.Wabel Abdallah, ni miongoni mwa waliouawa
Katibu mkuu huyo amelaani vikali shambulizi hilo akisema mashambulizi ya aina hiyo yanayowalenga raia kamwe hayawezi kukubalika na yanakiuka sheria za kimataifa.

                  MWISHO




18.01.2014        SAA 1:00 USIKU      MAZUNGUMZO
MOSCOW
Matayarisho ya mkutano wa wiki ijayo kusaka amani nchini Syria, yanaelezwa kufikia hatua nzuri, ambapo Waziri wa Mambo ya Nje Walid Mualle ametangaza mpango wa kubadilishana wafungwa na waasi wa nchi hiyo.
Muallem amesema, ameikabidhi serikali ya Urusi mipango ya usitishaji mapigano katika mji mkubwa zaidi wa Aleppo, na kwamba serikali yake iko tayari kubadilishana orodha na makundi ya waasi juu ya uwezekano wa kubadilishana kwa wafungwa.
Suala muhimu katika matayarisho ya mkutano huo, limekuwa ushiriki wa Iran, ambapo Urusi inataka Iran iwemo kwenye mazungumzo, huku mataifa ya Magharibi yakiishutumu nchi hiyo kuusaidia  utawala wa Assad na makundi yake.
Aidha makundi ya upinzani ya nchini Syria, ambayo yamekuwa yakishindwa kuwa na msimamo wa pamoja, yanakutana leo mjini Istanbul, Uturuki, kuamua ikiwa yashiriki au yasishiriki kwenye mazungumzo hayo ya amani yanayoihusu nchi ya Syria.
                      MWISHO






No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.