VYANZO VYA MAJI VYA MAPOROMOKO VILINDWE


SERIKALI imeshauriwa kulinda vyanzo vya maji vya asili vinavyotokana na maporomoko ya maji vinavyosaidia uzalishaji wa Nishati ya Umeme, hususani vilivyopo katika Bwawa la Kidatu na Mtera, ili
kuepusha uanzishwa au matumizi ya  vyanzo vingine vinavyochangia ongezeko la uzalishaji wa hewa ukaa na gesi joto kwa wingi duniani na hata kuharibu Tabaka la Ozoni (Ozone layer).

Ushauri huo ulitolewa na Meneja Uhifadhi wa Mfuko wa Uhifadhi wa mazingira duniani (WWF), upande wa Tanzania, Gerald Kamwenda, wakati akizungumza na wadau wa nishati na mazingira wanaokutana mjini Morogoro, ambapo alisema hewa ukaa na gesi joto, vimekuwa vikisababisha mabadiliko ya tabia nchini ikiwemo kuongezeka kwa joto la dunia, lakini dunia itaweza kuokolewa iwapo jitihada zitaongezwa kwa kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kutumia nishati Jadilifu kwa matumizi ya kila siku.

Alisema nishati jadilifu zinaweza kupatikana kutokana na mazingira mbalimbali kama upepo, kinyesi cha wanyama na umeme wa maji, ambao umekuwa ukisaidia kupatikana kwa nishati safi isiyo na athari kimatumizi, tofauti na umeme wa mafuta, ambao nguvu zake zimeendelea kuelekezwa na Serikali katika maeneo kama ya Kinyerezi, ambao huchangia uzalishaji wa gesi joto duniani.

Alibainisha kuwa Hewa ya ukaa inayotokana na mafuta ni mbaya zaidi ikilinganishwa na ile inayotokana na gesi, kwahiyo ni vyema Serikali ikaendelea kutilia nguvu katika utunzaji wa vyanzo vya maji vya mabwawa ya Kidatu na Mtera ambayo ni vyanzo vya asili, ingawa kwa kiasi Fulani vyanzo vinavyopeleka maji katika mabwawa hayo vinaathiriwa na mpango wa kilimo kwanza, kwa wananchi jirani na mito kama Ruaha uliotegemewa kutiririsha maji mwaka mzima,kuziba maji hayo  badala yake kuyaelekeza yasaidia kilimo kwa njia zisizo endelevu.

Alisema baadhi ya nchi dunia zimeweza kupiga hatua katika matumizi ya Nishati Jadilifu, na kwamba hata kwa Tanzania itawezekana iwapo kila mdau zikiwemo asasi za kiraia na Taasisi za Kiserikali, watashirikiana kubaini mambo mbalimbali yakayosaidia kukabiliana na uharibifu wa mazingira, gharama nafuu ya vifaa na miundo mbinu ya nishati jadilifu kama nishati ya jua, nishati ya upepo, nishati ya maji na nishati ya kinyesi (mbolea).

“Kwa kutumia nishati Jadilifu, inasaidia pia kutekeleza nguzo kuu tatu za MKUKUTA yaani kukuza uchumi na kupunguza umaskini, ustawi wa jamii na maisha bora kwa kila Mtanzania na hata suala zima la Utawala Bora”Aliongeza Meneja huyo wa Uhifadhi wa WWF.

Kwa upande wao Meneja Mradi wa Mafuta (Oil Project) wa WWF, Theresia Ole Mako, na Afisa Programu wa WWF Tanzania, Novat Kessy,walibainisha mfuko huo umebuni mradi utakaotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2014 hadi 2016, ukilenga kuangalia kanda ya Afrika, ili kuhakikisha nishati Jadilifu inafikiwa na watu wengi.

Ole Mako alishauri uwepo wa madawati ya Nishati hadi katika ngazi ya wilaya kama ilivyo kwenye maeneo mengine kama Kilimo, Maliasili, Ufugaji, Michezo na Utamaduni, badala ya suala hilo kubaki makao makuu pekee, ili kusaidia utekelezaji na usimamizi mzuri wa sera zinazohusu masuala ya Nishati na Mazingira.

Alisema nia ya mradi huo ni kuhakikisha asasi za kijamii zinaweza kuwafikia wanaotumia nishati hiyo, kwa kuangalia nishati zinazotumika katika maeneo husika, fursa rahisi zilizopo katika maeneo mbalimbali kama upepo, jua, vinyesi vya wanyama na fursa nyingine, na jitihada zinazofanywa kuhakikisha mazingira yanahifadhiwa na kupunguza mabadiliko ya hali ya hewa.

Alisisitiza kila mtanzania anapaswa kuhakikisha mazingira yanakuwa salama hata kwa kizazi kijacho, bila kujali atanufaikaje na usalama anaoutengeneza sasa, kupunguza matumizi ya mkaa ambayo yameonekana kuwa makubwa na mkaa kuvunwa kwa wingi kuliko unavyohifadhiwa, namna gani mtanzania hata wa hali ya chini ataweza kupata vifaa vya matumizi ya nishati jadidifu kwa matumizi ya kawaida.

Alizishauri Asasi za Kiraia kushirikiana na taasisi za Kiserikali ili kuwa na namna bora ya kufikia malengo ya pamoja hasa katika matumizi endelevu ya nishati Jadidifu.

No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.