Serikali ya shirikisho ya Somalia yakosolewa juu ya namna inavyoshughulikia siasa za dola ya Kusini Magharibi

Wasiwasi kati ya vikundi viwili vyenye siasa tofauti huko Baidoa, vinavyoongozwa na Mohamed Haji Abdinur na Madobe Nunow Mohamed, vimefikia hatua mpya baada ya serikali ya Somalia kutangaza mpangilio wa makubaliano baina ya pande mbili hizo katika mkutano ambao Mohamed hakuwepo.
Askari wa Ethiopia wanaohudumia chini ya Misheni ya Umoja wa Afrika nchini Somalia (AMISOM) wakitembea kuelekea Baidoa, Somalia, tarehe 22 Juni wakati wa kupiga doria katika jiji hilo. [AMISOM Photo / Tobin Jones]
Abdinur na Mohamed wamekuwa katika kutoelewana juu ya uundaji wa Dola mpya ya Kusini Magharibi ya Somalia tangia Machi, wakati wawili hao walipochaguliwa kuwa marais kutokana na pande mbili zenye ushindani huko Baidoa, moja ikiwa na mamlaka ya dola tatu Bay, Bakol na Shabelle ya chini, na nyingine ikitoa mwito wa dola mpya inayojumuisha pia Gedo, Jubba ya chini na Jubba ya kati, ambazo zilizungana kuunda Utawala wa Muda wa Jubba (IJA) mwaka uliopita.
Lakini tarehe 23 Juni, Serikali ya Somalia ilitangaza kwamba rais wa dola ya mikoa mitatu, Abdinur, na wawakilishi kutoka dola pinzani za mikoa sita inayoongozwa na Mohamed walifikia muafaka na kutia saini makataba huko Mogadishu kuunda kwa pamoja utawala wa muda wa mkoa ikiwa na mamlaka ya kisheria juu ya Bay, Bakol na Shabelle ya chini.
Hatahivyo Mohamed, alitupilia mbali mkataba huo, akiuita "batili" kwa sababu waziri aliyeutia saini kwa niaba yake, Abdifatah Mohamed Ibrahim, hakumwakilisha na alishaondolewa kwenye majukumu yake kabla ya kushiriki katika majadiliano hayo.


Mazungumzo zaidi, usuluhishi unahitajika
Mkataba huo umekumbana na ukosoaji mkubwa kutoka kwa viongozi wa koo na wanasiasa ambao walitoa wito kwa serikali ya shirikisho kutangua mkataba huo na kuwezesha mazungumzo zaidi kuhakikisha ushiriki wa wadau wote katika mchakato wa usuluhishi.
Raia pia walipinga makubaliano, wakiwa na siku tatu mfululizo za maandamano ya umma huko Baidoa ambayo yalimalizika kwa kuanza kwa Ramadan tarehe 29 Juni.
"Uamuzi wa serikali [kutambua dola tatu za kanda] hautafanya kazi kwa sababu ni kinyume cha katiba," alisema Hassan Elmi Yahya, mmoja wa wazee wa ukoo wa Hawiye. "Katiba inaeleza kwamba mikoa miwili au zaidi ambayo iko katika makubaliano inaweza kuanzisha dola ya shirikiso, lakini watu wa Shabelle ya Chini hawako tayari kujiunga na Bay na Bakol."
"Kuna vita vya [ukoo] vinavyoendelea katika Shabelle ya Chini. Inahitaji usuluhishi, kwa hiyo, watu lazima kwanza wapatane," aliiambia Sabahi.
Kwa upande wake, Mohamed, rais wa dola sita za kanda, alisema suala kuu lililopo ni namna ya kuhakikisha kwamba watu kutoka katika koo zote ambao wanatoka katika kanda sita zinazohusika wanaweza kushiriki katika siasa na wanawakilishwa katika serikali zao za mitaa.
Kabla ya kufikia mafikiano, alisema, mazungumzo zaidi yanatakiwa na IJA. "Hii inaweza kusababisha makubaliano ya namna ya kubainisha [na kulinda haki za] watu wanaoishi Jubba ambao tunashirikiana jadi zetu na watu kutoka Jubba wanaoishi Bay, Bakol na Shabelle ya Chini," Mohamed aliiambia Sabahi.
Makubaliano yaonyesha kutoafikiana katika serikali ya shirikisho
Makubaliano ya ubishi pia yamesababisha mgawanyiko ndani ya serikali ya shirikisho ya Somalia, pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani na Mfumo wa Shirikisho Abdullahi Godah Barre akipinga dhidi ya hatua hiyo, akiiita kinyume cha katiba na ya haraka.
"Hadi sasa, Baraza la Mawaziri halijakubaliana kuhusu sheria inayoeleza utaratibu wa kuanzisha uongozi wa mkoa," Barre alisema katika mahojiano na Idhaa ya BBC Somalia, akiongeza kwamba suala hilo linapaswa kusubiri hadi serikali itakapofanya uamuzi wa wazi kuhusu mchakato wa kuanzisha dola ya shirikisho.
Barre pia alisema wizara yake haikuwa imeambiwa kuhusu makubaliano na kwamba makubaliano kama hayo yanadhoofisha kazi ya wizara.
Hata hivyo, Waziri wa Michezo na Vijana Khalid Omar Ali, ambaye alipewa kazi ya kuongoza mazungumzo kati ya makundi mawili huko Baidoa kwa niaba ya serikali ya shirikisho, alitupilia mbali ukosoaji wa Barre na alisema kulikuwa hakuna ugomvi miongoni mwa viongozi katika serikali ya shirikisho kuhusu jinsi ya kushughulikia hali ya Baidoa.
"Rais, spika wa bunge na waziri mkuu wote walikubali. Uongozi wa nchi umefikia muafaka kuhusu makubaliano na baraza la mawaziri limeidhinisha. Wote kwa pamoja wasingeweza kukubaliana katika hilo kama kungekuwa ni kitu kisichofaa," aliiambia Sabahi.
Kinachotakiwa kufanyika
Mwenyeji wa Baidoa Ibrahim Ali Ahmed, ambaye alifanya kazi kama Mkuu wa wilaya ya Zaila chini ya utawala wa Mohamed Siad Barre, alisema njia pekee ambayo serikali ya mikoa hiyo mitatu inaweza kufanikiwa ni kupitia mazungumzo na usuluhishi zaidi.
"Kwanza wanatakiwa kukaa pamoja na kumridhisha raisi wa mikoa hiyo mitatu, Madobe Nunow [Mohamed]. Wanatakiwa pia kupatana na umma. Hicho ndicho kitakacholeta suluhisho," aliiambia Sabahi. "Hakuna jambo jingine litakalofanya kazi isipokuwa kama litaanzishwa kwa mazungumzo na usuluhishi."
Ahmed pia aliwaagiza viongozi wa serikali ya mikoa hiyo mitatu kuhakikisha koo zinazodharaulika zinazoishi katika mikoa hiyo zinahusishwa katika uundaji wa utawala wa serikali mpya.
Waziri wa Mipango na Ushirikiano wa serikali ya mikoa mitatu Mohamed Abdullahi Mursal alisema viongozi kutoka katika serikali yake wanapanga kufanya mazungumzo na koo zote zinazohusika kama sehemu ya makubaliano.
"Matakwa ya Somalia hayaegemei katika migogoro mipya," aliiambia Sabahi. "Tutampatia kila mmoja katika mkoa fursa ya kuwa sehemu ya utawala. Tutazungumza na kila mmoja na mlango wa mazungumzo utabaki wazi kwetu."
Mursal alisema wangeimarisha utawala shirikishi kwa watu wote wanaoishi katika mikoa hiyo mitatu na kwamba muda wa kuchukua mambo kwa nguvu umepita.
"Tumeibuka kutoka katika vita vya wenyewe kwa wenyewe na hatutarejea nyuma katika hilo. Tunaahidi kuona katika meza ya mazungumzo mtu yeyote ambaye hatafuti kufaidika kutokana na vita na mtutu wa bunduki," alisema.

No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.