TAARIFA RASMI KUHUSU TUKIO LA BINTI WA MIAKA 25 KUFARIKI DUNIA BAADA YA KUANGUKIWA NA JABALI WAKATI AKICHIMBA KOKOTO KAHAMA

Mkazi wa kijiji cha Shunu kata ya Nyahanga Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga, Lucia Bahati (25) amefariki dunia papo hapo baada ya kuangukiwa na jiwe katika eneo lililokuwa likitumika kutengeneza kokoto kijini humo.

Afisa mtendaji wa kata ya Nyahanga, William Upamba akiutazama Mwili wa Marehemu Lucia Bahati ukiwa umelazwa pembeni baada ya kutolewa ulipokuwa umepanwa na jiwe hilo kubwa.
 
Tukio hilo limetokea leo majira ya saa nne asubuhi wakati Lucia na wenzake wakichimba kokoto katika eneo hilo lililopo katika kitongoji cha Ikorongo ambalo liliwekwa mashine za kutengeneza kokoto wakati wa ujenzi wa Barabara za lami wilayani Kahama.

Kwa mujibu wa Angela Alex ambaye walikuwa wakichimba kokoto katika eneo hilo na Marehemu, jiwe hilo lilikuwa limekaa vibaya na kwamba walikuwa wakifanya kazi kwa tahadhari kabla ya kumuangukia mwenzake.

Afisa mtendaji wa Kijiji cha Shunu Benjamin Makelo, amesema baada ya tukio hilo, wananchi walifika kusaidia kusogeza jiwe hilo na kuutoa mwili wa Lucia ambaye ni mzaliwa wa Ilogi wilayani humo, akiwa tayari ameshafariki.
Afisa mtendaji wa Kijiji cha Shunu Benjamin Makelo akielezea tukio hilo lilivyokuwa.
Makelo amesema awali baada ya kupata taarifa za tukio hilo alipiga simu polisi ambao baadae walifika na kuuchukua mwili wa marehemu ambao sasa umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya wilaya ya Kahama.

Kufuatia tukio hilo, Afisa mtendaji wa kata ya Nyahanga William Upamba amesitisha shughuli za uchimbaji wa kokoto katika eneo hilo ambalo ni hatari kwa maisha ya watu, na ametoa siku 10 kwa wenye kokoto zao kuhakikisha wameziondoa.
Wananchi wakiangalia jiwe lililomwangukia na kumfunika Marehemu Lucia Bahati.

No comments

Theme images by sbayram. Powered by Blogger.