Isome katiba ya ndoa
Unajua katiba? Ni muundo wa sheria, kanuni zinazoainisha jinsi ambavyo nchi, chama au shirika vitakavyoendesha shughuli zao. Uhusiano wa kimapenzi upo katika mtindo wa kitaasisi lakini kwa bahati mbaya katiba yake haipo kwenye maandishi (non-written constitution).
Makala haya yataiweka katiba hiyo kwenye maandishi kwa ajili ya kukusaidia msomaji wangu kujua jinsi ya kuishi ndani ya uhusiano wako. Wengi wamekuwa wakipata tabu, wanapotoka na kuishi nje ya mistari inayofaa kwa sababu hawajaisoma au hawaijui.
Unahitaji muongozo wa kikatiba ili mapenzi yako yasitawaliwe na migogoro. Unatakiwa ujue jinsi ya kuishi kwa upendo na furaha. Amani itawale kwenye uhusiano, hali kadhalika tabia zako zikidhi mahitaji ya katiba ya mapenzi au ndoa yako.
Je, unatakiwa uyafanyie nini mapenzi yako au ndoa yako? Muonekano wako uweje mbele ya mwenzi wako? Ukiwa na hasira, ni kitu gani cha kufanya? Inapotokea mpenzi wako ameghadhabika, jambo lipi ufanye liweze kumrudisha kwenye mstari unaotakiwa?
Ndoa inahitaji nini? Kwa nini aliye kwenye ndoa hatakiwi kujiona ana uhuru wa kupitiliza kiasi cha kumuathiri mwenzi wake? Nini wajibu na haki za mtu kwenye mapenzi? Ni kwa namna gani mtindo wa maisha wa bachela, ukitekelezwa na mwanandoa ni sumu?
Hayo na mengine mengi, yanachambuliwa kinagaubaga kwenye katiba ya mapenzi. Mtu sahihi ni yule anayeishi kwa kujiamini, si ambaye anafanya kwa kujaribu, akisubiria matokeo au mapokeo ya mpenzi wake. Mapenzi ni rahisi mno endapo utaheshimu muongozo.
Katiba yenyewe inaundwa na vipengele vingi ambavyo nitavichambua katika wigo mpana ili uweze kuelewa ipasavyo. Inahitaji utulivu na umakini wakati wa kusoma, mwisho utakuwa ni mwenye mafanikio makubwa endapo yaliyomo kwenye maandishi yangu yatakita vilivyo ndani ya ubongo.
UPENDO
Hiki ni kipengele kikuu. Unaweza kukiita kifungu mama ndani ya katiba ya mapenzi. Huwezi kusema upo kwenye uhusiano makini kama upendo haupo katikati. Chukua hatua madhubuti endapo utabaini upendo haupo.
Mkatae mwenzi ambaye hakupendi, kinyume chake atakupa mateso mbele ya safari.
Muongozo wa kipengele cha upendo ni kwamba lazima wewe mwenyewe uanze kuwekeza upendo kisha naye akupende.
Ni maisha ya ubinafsi kutaraji kupendwa, wakati wewe mwenyewe huoneshi kwa mwenzako. Zingatia hili kila siku na wakati wote ili uweze kufaidi matunda mema kwenye uhusiano wako.
Kuna tabaka la watu ambao huishi kwa kusikilizia zaidi.
Haitakiwi kutegea, upendo unamaanisha pande mbili zinazovutana. Huyu anatekeleza hili kwa ajili ya mwenzake, hali kadhalika na mwingine anasimama imara kuhakikisha mpenzi wake anafaidi malisho mema ya mapenzi. Hakikisha mpenzi wako hakushindi upendo, onesha unampenda zaidi.
Upendo huyeyusha mengi. Ukiwekeza upendo kwa mwenzi wako, utamfanya nafsi yake iwe na woga. Ni rahisi kushinda vishawishi, kama atakuwa akikaa peke yake anakuwa anajiridhisha kuwa unampenda kwa moyo wako wote. Vinginevyo, anaweza kushawishika na kukusaliti kama tu akili yake itamtuma kuamini kwamba humpendi.
Hivyo basi, hakikisha upendo wako si wa wasiwasi. Mfanye awe na imani, ikibidi imani ya kupitiliza. Utafiti unaonesha kuwa mtu aliyeonesha upendo mkubwa kisha akasaliti kwa tamaa zake, anapobainika na kuachwa hujuta zaidi kuliko yule aliyeona hakukuwa na upendo kwa sababu haoni cha kupoteza.
TAMBUA MAKOSA YAKO
Hii ni lugha nzuri mno kwenye mapenzi. Unatakiwa kutambua makosa yako haraka na kutafuta njia ya kusuluhisha. Ukijielewa kwamba umekosea halafu ukakaa kimya hutoa ishara mbaya mbele ya safari.
KUWA MWEPESI KUSEMA SAMAHANI
Kiingereza kinatawala sehemu kubwa ya mawasiliano ya Watanzania, kwahiyo ukiona samahani utaonekana upo kienyeji, basi sema I am sorry. Hii ni baada ya kutambua makosa na unapoomba msamaha umaanishe kutoka moyoni.
USINUNE AKINUNA
Ni lugha ya mapenzi kwamba mwenzako akinuna, wewe jishushe ili mpate muafaka. Nyote mkigoma mtafika saa ngapi? Ni kosa kubwa unapobaini mwenzi wako ana hasira, nawe ukapandisha jazba kwani ni kiashiria cha kuachana.
CHUKIA ASIYOYAPENDA
Inafundishwa kwamba rafiki wa rafiki yako ni rafiki yako. Adui wa rafiki yako ni adui yako. Rafiki wa adui yako ni adui yako. Adui wa adui yako ni rafiki yako. Falsafa hii ikupe somo kwamba hutakiwi kupenda yale ambayo anayachukia.
Haikubali mtu ambaye hana jema kwa mwenzi wako, wewe umfanye rafiki. Fikiria upande wako kwamba kuna mtu anakula yamini kukumaliza, halafu ugundue kwamba mpenzi wako huwa anaketi naye na kuzungumza kwa kugongeshana mikono? Heshimu hisia za mwenzako.
ONGEZA MAPENZI KWA ANAYOPENDA
Mapenzi ni sanaa, ukiweza kucheza karata zako mtadumu bila kuchokana. Umeweza kuchukia yale ambayo hayapendi, sasa ni vizuri kuongeza mapenzi kwa yale ambayo anayapenda. Hii itasaidia kuwafanya muonekane ni kitu kimoja daima.
Hata hivyo, iga kwa mambo mazuri, isije ikawa mwenzako ni mtu wa baa kwa sana halafu na wewe umuige. Anapenda siasa, mpe ushirikiano nawe uipende taratibu. Mpira nenda mkaangalie pamoja, muvi na mengineyo, hayo ndiyo mapenzi.
MFANYE AKUTAMANI MUDA WOTE
Ni rahisi, unapokuwa naye muoneshe mapenzi ya dhati. Hakikisha hakasiriki mkiwa pamoja, yanayomhusu unabeba kama yako. Humkaripii na unamfanya yeye ni bora. Msifie kwamba ni mzuri na umueleze kwa hisia jinsi unavyomkubali. Hiyo itamfanya ajenge imani kubwa kwako na ukiwa mbali atajiona pungufu.
USITHUBUTU KUPAYUKA
Hata kama mmegombana, linda sauti yako. Tumia hekima na myamalize kimyakimya.
SWEETHEART, DARLING, BABY, HONEY, DEAR
Mpe heshima yake na umuoneshe ni kwa kiasi gani alivyo na nafasi kubwa kwako. Usipende kumuita kwa kumtaja jina lake au wengine wakishapata mtoto ndiyo utasikia “Mama Chausiku!” au “Baba Semeni!”
Haifai, tumia majina hayo au ukiweza tumia mengine yenye mvuto. Ikupe raha kutamka na yeye imfanye afurahi kusikia kutoka kwako. Mapenzi ni rahisi, utundu kidogo utakufanya uone dunia yote unaimiliki wewe.
Endelea kuwa nami kwa kulike Mr Clever Blog facebook, Twitter na Instagram
Leave a Comment